ENEO LA 1

1.7 Taarifa za umma zinapatikana kwa urahisi kwa
umma na zinatambulika kisheria
Baada ya miaka mingi ya ushawishi wa vyombo vya habari na watetezi wa haki
za binadamu, hatimaye Tanzania ilipitisha Sheria ya Upatikanaji wa Habari ya
mwaka 2016. Kifungu cha 5(1-3) cha sheria hiyo kinasema kwamba:
Kila mtu atakuwa na haki ya kupata habari ambayo iko chini ya udhibiti
wa mwenye habari hizo. Mmiliki wa habari, kwa mujibu wa Kifungu
cha 6 na sheria nyinginezo zozote zilizo kwenye maandishi, atatoa
taarifa kwa umma au, akiombwa kufanya hivyo, kwa mtu yeyote,
taarifa anazozimiliki yeye. Hakuna chochote katika Sheria hii ambacho
kitakwamisha au vinginevyo kuzuia matakwa ya sheria nyingine yoyote
ya mamlaka ya umma kutoa taarifa.
Sheria hiyo (Kifungu cha 7-9) kinabakiza kanuni za wajibu wa kutoa taarifa,
wajibu wa kutunza taarifa na wajibu wa kuandika taarifa fulani. Miongoni mwa
vifungu vingine, sheria inazitaka mamlaka kuteua maafisa habari kwa ajili ya
‘kushughulikia maombi ya taarifa na kutoa usaidizi kwa mtu anayetafuta taarifa
hizo’. Sheria inabainisha taratibu za kupatiwa taarifa kwenye Vifungu vya 10
na 11, ambazo ni pamoja na kutoa kipaumbele kwa watu wasiojua kusoma na
kuandika na watu wenye ulemavu.
Pamoja na hatua hizi chanya, washiriki walisema kwamba Sheria ya Upatikanaji
wa Habari bado haijitoshelezi. Mathalan, hakuna uwajibikaji kwa wamiliki wa
habari ambao hawataheshimu maombi ya habari. Walifanya ulinganisho na
India ambapo sheria kama hiyo inasema kwamba afisa habari atakayeshindwa
kuheshimu maombi ya habari anawajibika kama yeye. Sheria ya Tanzania pia
inawapa maafisa habari au watu wanaokaimu nafasi hizo, hadi mwezi mmoja ili
kujibu maombi ya habari, na hivyo kuweka kigingi kwa watu ambao wanaoweza
kuhitaji habari kwa haraka kama vile wanahabari na wanasheria. Aidha, Kifungu
cha 18 kinaweka mipaka kuhusu namna ambayo habari zilizotolewa zinaweza
kutumiwa, na kueleza muda wa kifungo cha hadi miaka miwili jela kwa mtu
atakayekutwa na hatia ya kubadilisha habari zilizopatikana kwa njia ya ombi la
Uhuru wa Habari (FOI).
Tangu Sheria ya Upatikanaji wa Habari ilipopitishwa, wanajopo wanasema
kwamba, kwa mshangao, upatikanaji wa habari umekuwa mgumu zaidi kwa
umma na kutolea mfano tafiti mbili zilizofanywa na Taasisi ya Vyombo vya Habari
Kusini mwa Afrika (MISA) na Baraza la Habari Tanzania, ambazo zilionesha
kwamba sheria hii haijaboresha upatikanaji wa habari. Washiriki walieleza
kwamba kwa utaratibu wa kuteua maafisa habari, baadhi ya mamlaka za
umma – kama vile serikali za mitaa, ambazo kiasili huwasiliana na wapiga kura,
wameacha utaratibu wao wa kutumia mbao za matangazo na njia nyinginezo
za mawasiliano. Kumekuwepo pia na kushuka kwa haraka kwa upatikanaji wa
habari kwenye tovuti za kiofisi na mitandao mingine ambayo ilikuwepo chini
ya utawala wa uwazi kabla ya mwaka 2016. Badala ya kuendeleza, washiriki
waliona kwamba Sheria ya Upatikanaji wa Habari ilikuwa imeweka vikwazo kwa
upatikanaji wa habari.

22

KIPIMO CHA VYOMBO VYA HABARI BARANI AFRIKA TANZANIA 2019

Select target paragraph3